News Details

Event

Rc Mbeya Aongoza Harambee Kuchangia Ujenzi Wa Hosteli Za Wasichana Chuo Kikuu Mzumbe

29 May Joseph Kiphizi Mon 29 May 2023

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Zuberi Homera ameongoza mamia ya Wadau wa maendeleo wakiwemo Viongozi wa Serikali,Wafanyabiashara, Wafanyakazi,Wanafunzi na Wananchi wa kawaida jijini Mbeya ili kuchangia harambee ya ujenzi wa hostel za wasichana katika chuo Kikuu Mzumbe, Ndaki ya Mbeya.
Akitangaza kiasi kilichopatikana katika harambee hiyo iliyofanyika Mei 25,2023 katika hoteli ya Eden jijini Mbeya, Mhe.Homera alisema kuwa jumla ya kiasi Shilingi 100, 705, 200 zimekusanywa na kufafanua kuwa fedha hizo ni makusanyo kutoka kwa makundi tofauti ya wachangiaji huku akitaja mchanganuo kuwa ni ahadi kiasi cha shilingi 48, 460, 000, mchango wa wadau katika matembezi ya hisani Sh 1, 466,100, mauzo ya vikoba Sh. 850,000, tukio la kupiga picha Sh. 320,000, mauzo ya fulana shilingi 330,00, matembezi ya asubuhi Shilingi 947, 800, michango ya Wafanyakazi (Staff) Shilingi 43, 331, 300.
"Tukio hili la kihistoria la kukusanya michango ya ujenzi wa hosteli katika chuo kikuu Mzumbe ni kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya Sita chini ya Rais wetu makini Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha elimu ,hivyo Wadau wote na wapenda maendeleo tujione tuna wajibu katika kukamilisha adhma hii na niziombe Wilaya zote pamoja na halmashauri zake kupitia Wakurugenzi kuchangia harambee hii ili kuhakikisha tunafikia malengo kwa wakati" amesema Mhe.Homera.
Kwa upande wake Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe, Prof. William Mwegoha, amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe.Juma Zuberi Homera na timu yake kwa ujumla kwa ushirikiano na kujitoa kwa dhati kuhakikisha fedha za ujenzi wa hostel za wanafunzi zinapatikana na kueleza kuwa huo ni uzalendo wa kiwango cha juu kabisa
Prof. Mwegoha amesema kuwa huo ni mwanzo mzuri hivyo wanapokwenda mbele wanatarajia kupiga hatua kubwa ya kuitisha harambee ya kitaifa ili kufikia lengo la kukusanya fedha za ujenzi.
Amesema kuwa Chuo Kikuu Mzumbe wataendelea kushirikiana kwa pamoja na Mkuu wa Mkoa ili ujenzi wa hosteli hizo uweze kukamilika kwa muda unaotakiwa jambo ambalo litasaidia watoto kukaa katika mazingira tulivo na rafiki kwa masomo yao.
Prof. Mwegoha amesema kuwa jumla ya shilingi bilioni 5.8 zinahitajika kwa ajili ya ujenzi wa hostel ya wasichana katika Ndaki ya Mbeya na kuwaomba wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo pamoja na wananchi kwa ujumla kuendelea kuchangia harambee hiyo kupitia namba ya malipo (control number) 994180331310 ili kufikia lengo kwa wakati

0 Comments

No Comments at the moment